Jumatatu, 28 Desemba 2015

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KIKAO CHA KAMATI MAALUM YA NEC ZANZIBAR ILIYOFANYIKA AFISI KUU YA CCM KISIWANDUI TAREHE 27 DESEMBA, 2015.

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein leo, amekiongoza Kikao cha Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) Zanzibar. Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC wa Idara ya Itikadi na Uenezi Bibi Waride Bakari Jabu imesema kikao hicho cha kawaidi cha siku moja kilifanyika Afisi Kuu ya Chama hicho, iliyopo Mtaa wa Kisiwandui Mjini Unguja.

Kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, 2015.
1. Kikao pamoja na mambo mengine, kimempongeza kwa dhati kabisa Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, 2015 na kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Awamu ya Tano) baada ya kupata ushindi wa kishindo (58.46%) na hivyo kuweza kuendeleza wimbi la ushindi kwa CCM ndani ya Demokrasia ya Vyama vingi vya Siasa nchini. Aidha, kikao kimempongeza Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan, kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

2. Kikao kimefurahishwa, kuridhishwa na kufarajika na idadi kubwa ya wana CCM kwa kujitokeza kwa wingi katika Uchaguzi Mkuu wa Dola wa Oktoba 25, 2015 na hatimaye kumchagua kwa kura nyingi za ndio Mgombea wa Chama Cha Mapinduzi wa Kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli, pamoja na Wabunge.

3. Kikao kimewataka wana CCM kujiimarisha, kujiweka tayari na hatimaye kujitokeza kwa wingi katika Uchaguzi wa marudio, ili kukiletea ushindi wa kishindo Chama Cha Mapinduzi Zanzibar kuanzia Rais, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani wakati utakapowadia.

4. Kikao pia kimeridhia majadiliano yanayoendelea kuhusu hali ya Kisiasa Zanzibar yanayoshirikisha Viongozi kadhaa wakiwemo Marais Wastaafu wa Zanzibar Mhe. Ali Hassan Mwinyi, Mhe, Dkt. Salmin Amour Juma na Mhe, Amani Abeid Karume, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi,

Kuhusu Shughuli za Kimaendeleo.
1. Kikao kimepongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) chini ya Uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika kuwaletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii wananchi wake. Aidha, imempongeza Mhe. Dkt. Shein kwa kusimamia suala zima la Amani na utulivu wa nchi kwa kipindi chote cha miaka mitano iliyopita.

2. Sambamba na hilo, Serikali imetakiwa kuongeza juhudi na kubuni mikakati madhubuti itakayosaidia kwa kiasi kikubwa kuanzishwa kwa miradi (mipya) mbali mbali ya maendeleo Mijini na Vijijini Unguja na Pemba, ili kuinua mapato ya Taifa.

Kuhusu Uhai wa Chama (CCM).
Kikao kimetoa pongezi za pekee kwa Wajumbe wote wa Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Viongozi wa Chama na Jumuiya zake kwa kazi nzuri ya kuimarjisha Chama na kuwataka kuwa mstari wa mbele katika kukipigania, kukilinda na kukitetea kwa nguvu zote Chama hicho. Aidha, kimewataka kuendelea kufanya kazi kwa mashirikiano, juhudi na maarifa katika kukijenga na kukiimarisha Chama, kwa maslahi ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla.

 Mwisho, kikao hicho kilihudhuriwa na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan. Mwisho. Waride Bakari Jabu, Katibu wa Kamati Maalum wa NEC, Idara ya itikadi na Uenezi – CCM, ZANZIBAR. 27/12/2015.

Maoni 1 :