Jumatatu, 21 Novemba 2016

AWASIHI VIONGOZI WA CHAMA KUENDELEZA UTAMADUNI


Na Is-haka Omar, Zanzibar.


NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar ,  Nd. Vuai Ali Vuai amewasihi Viongozi  wa ngazi mbali mbali za Chama  kuendeleza   utamaduni  wa  kuandaa mafunzo ya kuwajengea uwezo Watendaji  wao ili wawe na uelewa  na ujuzi  wa kutekeleza shughuli za Chama kwa ufanisi.


Akizungumza katika Ufunguzi wa Mafunzo elekezi ya Watendaji  wa Chama na Makatibu wa Siasa na Uenezi kuanzia  ngazi za Matawi, Wadi hadi Jimbo  Wilaya ya Amani Kichama yaliyofanyika katika Hoteli ya Villa iliyopo  Maruhubi  Nje Kidogo ya Mjini wa Zanzibar.


Alisema mafunzo  ni nyenzo muhimu  inayosaidia  kuwaongezea maarifa na mbinu mbadala za  kiutendaji  watumishi na watendaji wa taasisi ili wafanye  kazi zao kwa kujiamini zaidi.


Vuai  Alifafanua kuwa CCM inakabiliwa na majukumu ya Uchaguzi wa Chama na Uchaguzi Mkuu wa Dola hivyo  watendaji wa chama hicho wanatakiwa  wanatakiwa kuandaliwa vizuri kupitia mafunzo ya chama kwa lengo la kukumbushwa baadhi ya majukumu yao ya msingi yakiwemo matumizi sahihi ya kanuni, katiba na miongozi ya Chama kwa makada wengine.


“Tuendelee kufanya mafunzo kwa  wingi kadri hali itakavyoruhusu  kwani  ni jambo muhimu kwa binadamu yeyote yule anayetaka maendeleo mazuri ya kazi yake  kwa lengo la kuongeza ujuzi na ufanisi  katika utekelezaji  wa shughuli  zetu za kisiasa ndani na nje ya Chama chetu.”, alisema Vuai na kuongeza kuwa mafunzo  yatawasaidia watendaji hao  kuelewa kwa upana  wanayoyafanya na kuepuka athari ya kufanya kazi kwa mazoea.


Naibu Vuai alieleza kwamba utaratibu wa mafunzo umeanza zamani  ambapo Chama kilikuwa na vyuo vyake maalum vya kuwaandaa makada , watendaji na viongozi makini waliokuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja  na kuzisimamia katika kuimarisha maendeleo ya Chama.


Alisema kwa mujibu wa ibara ya 5 ya Katiba ya Chama hicho ni kushika Dola Tanzania bara na Zanzibar serikali za mitaa na serikali kuu, hivyo amewapongeza  makada hao kwa uwezo na jitihada zao za kuahakikisha kila uchaguzi toka umeanza mfumo wa vyama vingi CCM imekuwa ikishinda.


Aidha aliwataka watendaji hao kuanzia ngazi za Matawi hadi Wilaya kutumia fursa walizokuwa nazo katika maeneo yao kwa kuanzisha miradi mbali mbali itakayowasaidia kupata kipato cha kutatua baadhi ya changamoto zinazohitaji fedha na kujitegemea wenyewe badala ya kuendelea kuwategemea  Viongozi wa majimbo pekee.


Hata hivyo aliendelea kuwakumbusha  washiriki wa mafunzo hayo kwamba  Watendaji watakaopata fursa ya kugawa fomu za kugombea Uongozi  ndani ya CCM waongeze bidii katika kutenda haki kwa kuhakikisha kila mwanachama  mwenye sifa ya kuchagua na kuchaguliwa  anapata haki hiyo kwa mujibu wa  ibara ya 14 ya Katiba ya Chama hicho.


“ Najua watendaji na viongozi wa CCM ni waadilifu lakini naomba tuongeze umakini katika suala la Uchaguzi wa Chama kwa kuwapatia fomu wale wote wenye Haki ya kuchagua na kuchaguliwa msiwanyime fursa hiyo  kama mtu hafai basi mwacheni  akanyimwe kura  na wanachama wenzake  lakini nyinyi msihusike  na kufanya hivyo kutapunguza malalamiko .”, alisisitiza Vuai.


Naye  Katibu wa Wilaya ya Amani Kichama, Abdallah Mwingi  amesema  lengo la mafunzo hayo kwa lengo la kuzidi  kuwajengea uwezo  watendaji hao ili waweze kusimamia ipasavyo Chaguzi za Chama na Dola zijazo kwa kuwachuja wanachama wanaotaka nafasi za uongozi na kuwapata viongozi ambao ni waumini wa dhati wa itikadi na sera za CCM na serikali zilizopo madarakani.


Alisema  Wilaya hiyo imekuwa ikifanya kazi ya ziada ya kuimarisha chama kwa kuongeza wanachama wapya na kuwapatia mafunzo maalum  kupitia madarasa ya itikadi kwa lengo la kuwajenga kuwa waumini wa kweli  watakaosimamia maslahi ya CCM bila ya hofu.


Akitoa maneno ya Shukrani Mbunge wa Jimbo la Mpendae, Salim Hassan Turky, amesema  washiriki hao watazifanyia kazi nasaha hizo kwa lengo la kuhakikisha CCM inaendelea kuwa Chama bora kinachokubalika kwa wananchi.


Aliwasihi  watendaji  hao  makundi ya kukigawa chama wakati wa Uchaguzi kwani  kuna baadhi ya watendaji waliowahi kusimamia chaguzi zilizopita wamekuwa wakilalamikiwa kwa kufanya upendeleo kwa baadhi ya Wagombea wanaowataka na hatimaye wanapatikana viongozi wenye sifa za kutilia shaka.


 Aliwaomba washiriki hao kuwasaidia na kuwaongoza   wanachama wa Chama hicho katika  kuanzisha miradi midogo midogo kuanzia ngazi za Mashina hadi Mikoa, itakayoweza kuwasaidia kujiajiri wenyewe na kukuza Uchumi wa nchi.